Upande wa Mashtaka katika kesi ya kughushi na kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu inayomkabili mfanyabiashara, Ndama Hussein maaru...
Upande wa Mashtaka katika kesi ya
kughushi na kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu inayomkabili
mfanyabiashara, Ndama Hussein maarufu Pedeshee Ndama mtoto ya Ng'ombe,
umeieleza mahakama kuwa wanasubiri nyaraka kutoka nchini Australia.
Ndama anakabiliwa na mashtaka matano ya
kughushi na kujipatia dola 540,000 za Marekani kwa njia ya udanganyifu
katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.
Wakili wa Serikali, Estazia Wilson
amedai leo Februari 12, 2018 mbele ya hakimu mkazi mkuu wa Mahakama
hiyo, Victoria Nongwa, kuwa wameshapeleka maombi kwa ajili ya kupata
nyaraka hizo.
Pia, wakili Wilson amedai kuwa mshtakiwa ni mgonjwa na leo ameshindwa kufika mahakamani hapo.
"Mheshimiwa hakimu, tunasubiri nyaraka
kutoka nchini Australia na mshtakiwa leo hajafika mahakamani kwa sababu
ni mgonjwa, hivyo tunaomba tarehe nyingine kwa ajili ya kutajaa,”
amedai.
Januari 10, 2018 kesi hiyo iliahirishwa
baada ya upande wa mashtaka kuieleza mahakama hiyo kuwa wanasubiri
nyaraka kutoka nchini Australia.
Kuhusu nyaraka, wakili Wilson amedai kuwa wanazosubiri ni zile walizoomba kutoka nchini Australia.
Hakimu Nongwa alikubaliana na ombi la
upande wa mashtaka na kuahirisha kesi hiyo hadi Februari 28, 2018
itakapotajwa na dhamana ya mshtakiwa inaendelea.
Ndama anakabiliwa na mashtaka matano
ambayo katika shtaka la kwanza, anadaiwa kuwa Februari 20, 2014 Dar es
Salaam, alighushi kibali cha kusafirisha madini na sampuli za madini
kwa kusudi la kuonyesha kuwa kampuni ya Muru Platnum Tanzania Investment
Company Limited iliruhusiwa kusafirisha maboksi manne ya dhahabu yenye
kilo 207 yenye thamani ya Dola 8,280,000 za Marekani kwenda Australia
kwa kampuni ya Trade TJL DTYL Limited wakati akijua si kweli.
Pia anadaiwa Machi 6, 2014, Dar es
Salaam, alighushi kwa kutengeneza hati ya kibali ya Umoja wa Mataifa
ofisi ya Dar es Salaam akijaribu kuonyesha kilo 207 za dhahabu kutoka
nchini Congo zinatarajiwa kusafirishwa na kampuni ya Muru Platnum
Tanzania Investment Company Limited kwenda Australia kwa kampuni ya
Trade TJL DTYL Limited, zimesafirishwa bila jinai yoyote wakati akijua
si kweli.
Katika shtaka la tatu, Ndama anadaiwa
Februari 20, 2014, alighushi fomu ya forodha yenye namba za usajili
R.28092 akionyesha kampuni ya Muru imeilipa Mamlaka ya Mapato Tanzania
(TRA) dola 331,200 za Marekani kama kodi ya uingizaji wa bidhaa ambazo
zina uzito wa kilo 207 za dhahabu zenye thamani ya dola 8,280,000 za
Marekani kutoka Congo.
Pia, anadaiwa kuwa Februari 20, 2014
alighushi nyaraka ya bima kutoka Phoenix of Tanzania Assurance Company
Ltd akionyesha kampuni ya Muru imeyawekea bima maboksi manne yaliyokuwa
na dhahabu hizo.
Anadaiwa kati ya Februari 26 na Machi 3,
2014, Dar es Salaam kwa njia ya udanganyifu alijipatia kutoka kwa
kampuni ya nchini Australia ya Trade TJL DTYL Limited dola 540,000 za
Marekani baada ya kudanganya atawapa na kusafirisha dhahabu hizo.
COMMENTS