MWALIMU Mkuu wa Shule ya Msingi Magu iliyoko Wilaya ya Magu mkoani Mwanza, Prosper Kagombolo amehukumiwa na Mahakama ya wilaya hiyo kw...
MWALIMU Mkuu wa Shule ya Msingi Magu
iliyoko Wilaya ya Magu mkoani Mwanza, Prosper Kagombolo amehukumiwa na
Mahakama ya wilaya hiyo kwenda jela miaka mitatu ama kulipa faini
isiyopungua laki tano kwa kosa la kuomba rushwa kwa mwanafunzi wake ili
aweze kumpatia cheti chake cha kuhitimu darasa la saba.
Hukumu hiyo ilitolewa jana na Hakimu
Mfawidhi wa Wilaya hiyo, Edmund Kente baada ya kuridhishwa na ushahidi
uliotolewa na upande wa ulalamikaji wakati walipokuwa wakieleza Mahakama
mazingira ya tukio. Mshtakiwa alipelekwa jela baada ya kushindwa kulipa
faini.
Mashahidi hao walieleza namna mwalimu
huyo alivyomuomba mwanafunzi wake rushwa ya Sh 50,000 ili aweze
kumsaidia kupata cheti chake huku akijua ni kinyume na taratibu za nchi
kupitia kifungu cha sheria namba 15 (1) cha Sheria ya Kuzuia na
Kupambana na Rushwa Namba 11 ya mwaka 2007.
Hakimu huyo aliiambia Mahakama kuwa
Serikali ya Awamu ya Tano ipo katika kuwatendea haki watu wanyonge,
hivyo watumishi wa serikali wasijione kuwa wako juu ya sheria kuliko
watu wengine na wanaweza kuvunja sheria na wasichukuliwe hatua kwa
kuogopwa kuwa ni watumishi wa serikali.
Aidha Kente aliwapongeza maofisa wa
Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) kwa jinsi
wanavyojitaidi kupambana na watu wanaokwenda kinyume na maadili ya kazi
za utumishi wa umma.
Akitoa ushahidi kwenye Mahakama hiyo ya
Wilaya, Mwendesha Mashitaka wa Takukuru Maximiliani Kyabona alisema kuwa
walipata taarifa za mwalimu huyo kuomba kiasi hicho cha fedha kutoka
kwa mwanafunzi wake aliyemfundisha miaka ya nyuma mara baada ya
mwanafunzi huyo kwenda shuleni hapo kuomba cheti chake.
“Mwalimu alimuomba kijana huyo kiasi cha
Sh 50,000 kwa lengo la kutaka kumsaidia, ndipo mwanafunzi huyo (jina
linahifadhiwa) alifika ofisini kwetu kuomba msaada juu ya jambo huilo,”
alisema.
COMMENTS